UCSAF kuwezesha wasichana wa kitanzania kufanikiwa katika TEHAMA

  • 06 September, 2023
UCSAF kuwezesha wasichana wa kitanzania kufanikiwa katika TEHAMA

Katika ulimwengu wa sasa ambao unabadilika kutokana na ukuaji mkubwa wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), wasiwasi mkubwa ni uwepo wa pengo la kijinsia ambalo linatenganisha wanaume na wanawake katika sekta hii.  Usawa wa kijinsia katika ulimwengu wa kidijitali ni muhimu na ili kuufanikisha zinahitajika jitihada za dhati za kuwawezesha wanawake na wasichana kuingia katika Sayansi, Teknolojia, Uhandisi, na Hisabati (STEM).  Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) umechukua hatua ya kuwalea mashujaa wa kike wa STEM ambao wanafanya vizuri katika nyanja za Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hesabu.

Kukuza vipaji na ubunifu

Mapema mwaka huu, UCSAF ilifadhili mpango wa mabadiliko uliowaleta pamoja wanafunzi 246 kutoka mikoa mbalimbali nchini. Vijana hawa walishiriki katika mafunzo na mashindano ya kikanda yaliyofanyika katika vituo vitatu ambavyo ni; Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) na Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST). Kwa muda wa siku tano, vituo hivi vilikuwa kitovu mahiri cha ubunifu na uvumbuzi huku wasichana wakiingia katika ulimwengu wa TEHAMA. Mafunzo hayo sio tu kwamba yalitoa maarifa ya kiufundi bali yalienda mbali zaidi kwa kujikita katika kujengea uwezo wa kujitambua na ujuzi muhimu kwa ajili ya ustawi katika tasnia ya TEHAMA.

Wasichana walihamasishwa kutumia uwezo wao, kukuza uhusiano thabiti na wenzao na kutumia mawazo katika kubuni. Masuala haya yalikuza ubunifu, yaliwezesha wanafunzi kutoa mawazo na masuluhisho ya msingi kupitia michoro, utayarishaji wa picha na tafakuri.

Mawazo yanayobadilisha maisha

Kiini cha mkakati huo kipo katika miradi ya programu ya simu iliyotengenezwa wakati wa mafunzo na mashindano ya kikanda. Miradi hii inathibitisha ustadi wa wanafunzi na azma yao ya kutatua changamoto zinazoukabili ulimwengu kwa kutumia teknolojia. Katika kituo cha UDOM, mradi wa kuleta mabadiliko uliopewa jina la "Mahudhurio App" ulilenga kushughulikia suala la utoro wa muda mrefu miongoni mwa wanafunzi wa kutwa.

Programu hii bunifu inajiendesha kiotomatiki kwa kufuatilia mahudhurio ya wanafunzi kisha hutuma taarifa kwa kutumia ujumbe mfupi wa maneno (SMS) kwa wakati moja kwa moja kwa wazazi au walezi, kuwafahamisha kuhusu kuwepo au kutokuwepo kwa mtoto wao shuleni. Mawasiliano haya yasiyoonekana yanawezesha ushiriki mkubwa wa wazazi katika ufuatiliaji wa mahudhurio ya wanafunzi kwa wakati ili kuhakikisha mafanikio ya kielimu ya mtoto.  

Kituo cha MUST kiliwasilisha "Programu ya kuripoti Unyanyasaji wa Kijinsia," suluhisho ambalo liliwapa waathiriwa uwezo wa kuripoti matukio ya unyanyasaji bila kujulikana utambulisho wao. Kwa kurahisisha mchakato wa kuripoti, programu hii inatoa jukwaa salama kwa watu binafsi kutafuta usaidizi na kutoa mwongozo kuhusu suala muhimu linalohitaji kushughulikiwa kwa haraka. 

Washiriki kutoka kituo cha DIT walionyesha ubunifu wao kupitia "Toto Lishe App," programu yenye nguvu inayolenga kupambana na utapiamlo miongoni mwa watoto walio chini ya umri wa miaka mitano. Programu hii inatoa maelezo ya lishe, vikumbusho vya milo na mfumo wa kufuatilia ukuaji wa mtoto ili kuwawezesha wazazi na walezi kufuatilia afya na mahitaji ya lishe ya watoto wao kwa ufanisi.

Mafunzo na mashindano ya kitaifa

Kilele cha Siku ya Wasichana katika TEHAMA kilifikiwa kwa kufanyika kwa mafunzo na mashindano ya kitaifa yaliyofanyika UDOM kuanzia tarehe 19 hadi 21 Machi 2023. Hapa, wanafunzi 31 bora kutoka mikoa mbalimbali nchini kila mmoja akiwakilisha mkoa wake, walishiriki katika hafla hiyo, huku kila kituo kikionyesha miradi yao husika. Miradi hii ilitathminiwa kulingana na ubunifu, uvumbuzi na athari zake kwa jamii.

Miradi iliyoibuka washindi ilikuwa ya kustaajabisha. "Mahudhurio App" kutoka kituo cha UDOM iliendelea kupata sifa kwa mbinu yake kuu ya kuleta mapinduzi ya mahudhurio ya shule na ushiriki wa wazazi katika elimu ya watoto wao. "Programu ya Kuripoti Unyanyasaji wa Kijinsia" kutoka kituo cha MUST iliendelea kutetea sababu ya kuwawezesha waathirika na kurahisisha mchakato wa kuripoti, kuangazia suala linalohitaji kushughulikiwa haraka na kuchukuliwa hatua.

"Toto Lishe App" kutoka kituo cha UDOM ilivutia watu wengi kwa umakini wake katika kuzuia utapiamlo kwa watoto. Vipengele vyake bunifu viliwawezesha wazazi kufuatilia afya za watoto wao na kuhakikisha milo inayofaa na yenye lishe kwa wakati na hivyo kupata mustakabali mzuri wa Taifa. Washiriki wa kituo cha DIT walionyesha uwezo wao kwa kupitia "Programu ya Huduma ya Afya," ambayo ni programu ya kuziba pengo kati ya mfumo wa huduma ya afya na umma. Programu hii iliwezesha ufikiaji rahisi wa huduma za afya kwa watu binafsi na kutengeneza jamii yenye afya na imara zaidi.

Programu ya "Mkulima App" kutoka kituo cha DIT iliibuka kuwa suluhu ya matumaini inayowaunganisha wakulima na watoa huduma wa bidhaa za kilimo, kuleta mapinduzi katika sekta ya kilimo na kuweka njia ya ukuaji endelevu.

Kusherehekea mashujaa wa kike wa STEM ambao ni washindi wa kitaifa

Hafla ya kuhitimisha sherehe hizo ilihudhuriwa na Mhe. Mhandisi Kundo Andrea Mathew (Mb), Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano, na Teknolojia ya Habari. Hafla hii ilikuwa ni sherehe ya furaha ya mafanikio ya mashujaa hao wa STEM. Kivutio kikuu kilikuwa wanafunzi sita bora walioibuka washindi katika shindano hilo la kitaifa, huku kila kituo kikitoa washindi wawili.

Hilkia Emmanuel Mafie kutoka Shule ya Sekondari Mringa ya Arusha, Getrude Charles Kaswaga kutoka Shule ya Sekondari Msalato ya Dodoma MC, Kahabi Jackson Derefa kutoka Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Iringa MC, Aneth Alinda Kayungi Sekondari ya Nyankumbu ya Geita TC, Loveness Greyson Hegani kutoka Mustafa Sabodo Sekondari ya Mtwara na Rayyan Hassan Bushir kutoka Sekondari ya Ben-Bella Mjini Magharibi walitambuliwa kwa mafanikio yao ya kipekee. Kama ishara ya shukrani, wanafunzi wote 31 walikabidhiwa kompyuta mpakato na mabegi ikiwa ni ishara ya kutambua umuhimu wao na kuwapa motisha ya kuendelea na harakati zao za fani za STEM.

Kufungua njia kwa mustakabali jumuishi

Ahadi ya UCSAF ya kuendelea kuwawezesha wanawake na wasichana katika tasnia ya TEHAMA, inaweka kielelezo kwa wadau wengine kuunga mkono juhudi hizo. Tunaposherehekea mashujaa hawa wa STEM, lazima tuendelee kutoa fursa, ushauri na kutetea usawa wa kijinsia katika nyanja zote.

Kwa kufanya hivyo, tunafungua njia kwa mustakabali jumuishi zaidi, ambapo wanawake na wasichana watasimama kwa fahari kama viongozi na wabunifu katika sayansi, teknolojia, uhandisi na hesabu na kuubadilisha ulimwengu kuufanya kuwa bora. Mashujaa hawa wa STEM sio tu wataboresha tasnia ya TEHAMA, lakini pia wataboresha mustakabali wa Taifa letu kwa ujumla.