UCSAF yawataka wadau kuchangamkia fursa zinazotolewa na Mfuko huo.

  • 15 September, 2021
UCSAF yawataka wadau kuchangamkia fursa zinazotolewa na Mfuko huo.

Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) umetoa wito kwa wadau wa Mawasiliano nchini wakiwemo wamiliki wa redio hasa radio jamii, runinga na huduma za waya (cable tv) kuchagamkia fursa zinazotolewa na Mfuko huo ili kuboresha usikivu wa vyombo vyao kwa lengo la kuwezesha watanzania wote kupata huduma bora za mawasiliano katika maeneo yao.

Hayo yameelezwa na Mhandisi Richard Sotery kutoka UCSAF katika mkutano wa siku moja kati ya taasisi hiyo na wadau wa mawasiliano kanda ya kati uliofanyika Mkoani Tabora, ukiwa na wadau kutoka mikoa ya Tabora, Kigoma na Singida.

Mhandisi Sotery ameongeza kuwa ni muhimu kwa watoa huduma za mawasiliano kuelewa malengo ya kuanzishwa Mfuko huo ili kutambua fursa zilizopo ikiwemo ruzuku ambayo hutolewa ili kusaidia kufikishwa kwa huduma za mawasiliano vijijini, kuboresha usikivu wa matangazo ya redio na runinga kwenye maeneo yenye usikivu hafifu na maeneo ya mipakani.

“Usikivu wa redio na mawasiliano ya simu bado ni changamoto katika maeneo mengi hapa nchini, natoa wito kwa watoa huduma za mawasiliano ikiwemo wamiliki wa redio kushirikiana na mfuko ili kwa pamoja tuhakikishe kuwa kila mtanzania anapata huduma hii muhimu kutoka kwa vyombo vya habari vya hapa nchini”. Alisema Mhandisi huyo.

Kwa upande wake Mhandisi Shirikisho Mpunji kutoka UCSAF akiwasilisha mada amesema, lengo lingine la kufanyika kwa mkutano huo ni kuwafahamisha wadau kuhusu haki na wajibu wao kwa Mfuko pamoja na kujenga mahusiano bora yatakayoiwezesha taasisi hiyo kufanya kazi kwa ukaribu na kwa kushirikiana na watoa huduma za mawasiliano.